Tuesday 29 August 2017

Ndikumana: Kumuoa Uwoya nikujitakia kifo

PICHA linaendelea! Baada ya hivi karibuni gazeti tumbo moja na hili, Risasi Mchanganyiko kufanya mahojiano maalum na staa mkubwa wa sinema za Kibongo, Irene pancras Uwoya na kudai kwamba amekuwa akitaka talaka yake kwa muda mrefu kutoka kwa aliyekuwa mumewe, hamad ndikumana ‘ndiku’ bila mafanikio, mwanaume huyo anaelezwa kutimiza matakwa hayo.

Inaelezwa kuwa, Ndiku aliridhia ishu hiyo huku akimpa tahadhari mwanaume atakayemuoa mwanamama huyo kuwa asipokuwa makini, basi atakuwa anajitakia kifo.

TUJIUNGE NA CHANZO
Chanzo makini kililieleza kuwa, tayari Ndiku ameshamwandikia Uwoya talaka ya kimahakama kwa kuwa wawili hao walifunga ndoa kanisani.

“Si unajua ndoa ya kanisani huwa hakuna talaka? Ndiku ameona bora afanye utaratibu huo wa kupitia mahakamani maana huko huwa hakuna kizuizi.

“Hapa tunapoongea tayari Ndiku ameshampa talaka Uwoya kwa sababu amevumilia na kupitia kwenye misukosuko mingi wakati akiwa kwenye ndoa na mwanamama huyo.

NDIKU FULU KUJUTA
“Ndiku amekuwa akijutia namna alivyoingia mkenge, akaweka maisha yake rehani hivyo hata kama Uwoya asingedai talaka, mwanaume huyo asingeweza kumrudia tena,” kilisema chanzo hicho na kuongeza:

“Ndiku anasema sasa Uwoya yupo huru kuolewa na mwanaume mwingine lakini anamuonea huruma atakayemuoa kwani atakuwa anajitakia kifo.

HAWEZI KUSAHAU KOSA?
“Katika maisha yake, Ndiku anasema hawezi kusahau kosa alilolifanya la kumuoa Uwoya maana alijikuta katika wakati mgumu, alikonda na kuna wakati hata alitaka kujitoa uhai.

“Ni mambo mengi aliyopitia na mara nyingi huwa hataki kukumbuka maana ilibaki nukta tu afe kwa presha. Kama mtu ajui maumivu ya mapenzi, basi amuulize Ndiku.

“Ndiku anamshauri mwanaume atakayemuoa Uwoya awe na roho ngumu mno la sivyo naye atajikuta kwenye maumivu kama aliyoyapitia yeye.

KINACHOMUUMIZA NDIKU
“Lakini kinachomuumiza zaidi Ndiku anasema ni mtoto tu aliyezaa na Uwoya maana atakapokuwa mkubwa atadhani yeye kama baba alimtelekeza lakini ukweli ni kwamba alitengana na mkewe kwa kushindwa kuvumilia maumivu aliyokuwa anakumbana nayo,” kilitiririka chanzo hicho ambacho ni ndugu wa familia ya Ndiku aishie jijini Dar.

IJUMAA WIKIENDA NA NDIKU
Baada ya chanzo kutiririka hayo, Ijumaa Wikienda lilimtafuta Ndiku kwa njia ya mtandao wa kijamii wa Instagram ambapo baada ya kuulizwa kuhusiana na ukweli juu ya masuala hayo yanayozungumzwa, alisema kuwa kwa miaka mingi alikuwa tayari kumpa talaka mzazi mwenzake huyo maana kilichokuwa kikimzuia kilishakwisha.

Alipoulizwa ni kitu gani kilichokuwa kikimzuia, Ndiku alisema kuwa, hawezi kueleza kwa kuwa wazazi wake wamemkataza asiseme hadharani na kwamba anawaheshimu kuliko kitu chochote ila watu wote wajue kwamba katika maisha aliyoishi na Uwoya, aliponea chupuchupu kupoteza uhai kutokana na mambo aliyokuwa akikutana nayo kwa mwanamama huyo.

KUMBE ALIKUWA TAYARI MIAKA MINGI
“Nipo tayari miaka mingi sana kutoa talaka maana kilichokuwa kinanizuia kilishaisha, kuna mtu wa mahakama nilimtuma ili akamilishe kila kitu kuhusu talaka ya Irene (Uwoya).
“Nilimwambia huyo mtu aniambie nini cha kufanya bila mimi kuja huko Tanzania (yupo nyumbani kwao nchini Rwanda) ili nimsainie hiyo talaka yake.
“Nimeponea chupuchupu na natamani niseme lakini ndiyo hivyo wazazi wangu wamenikataza na sijawahi kukataa kumpa Irene talaka,” alisema Ndiku na kuongeza:

TAHADHARI KWA MUOAJI
“Ninamtakia kila la heri atakayemuoa kwani kama hatakuwa makini atakuwa anajitakia kifo kama mimi nilivyoponea chupuchupu.”

WAMEFIKAJE HAPA?
Mwanasoka huyo wa zamani wa Rayon Sports ya nyumbani kwao, Rwanda na Uwoya walifunga ndoa mwaka 2009 na walibahatika kupata mtoto mmoja wa kiume kabla ya kutengana mwaka 2011 ambapo wiki iliyopita mwanamama huyo alilalama kuwa anahitaji talaka ili aendelee na maisha yake mengine.

Katika kipindi chote hicho alichokuwa kwenye mgogoro na Ndiku, Uwoya aliwahi kutajwa kutoka kimapenzi na mastaa wenzake wa Bongo Movies akiwemo Kulwa Kikumba ‘Dude’ na wengineo. Mbali na hao, Uwoya aliwahi kuhusishwa na ‘vitoto’ vya Bongo Fleva, Msami Baby na Dogo Janja kabla ya kutajwa kutoka na mwanamuziki wa nchini Kenya, Jaquar.