Tuesday 29 August 2017

Mwenyekiti wa Yanga apitishwa kuwania Uwenyekiti wa Bodi ya Ligi

Kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), imetangaza majina manane ya wagombea ambao yamepita katika mchujo wa awali kuwania nafasi mbalimbali katika Kamati ya Uongozi (Management Committee) ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara.

Waliopitishwa ni kuwania uenyekiti wa Management Committee ni Clement Sanga ambaye ni kaimu mwenyekiti wa Yanga na Ahmed Yahya anayeshikilia nafasi hiyo wakati Shan Crysostoms ameiptishwa kuwania nafasi ya makamu mwenyekiti.

Kwa mujibu wa kamati hiyo, Ramadhan Mahano na Hamisi Madaki wamepitishwa kuwania nafasi ya Ujumbe wakitokea klabu za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.

James Bwire na Almas Kasongo wamepitishwa kuwania Ujumbe wakitokea klabu za Ligi Daraja la Kwanza. Brown Ernest hakupitishwa kwa sababu hakuthibitishwa na klabu yake.

Edga Chubura amepitishwa kuwania ujumbe akitokea klabu za Ligi Daraja la Pili.

Wagombea kwa mujibu wa kanuni za uendeshaji wa Bodi ya Ligi Kuu ni marais au wenyeviti wa klabu husika. Wagombea wanatakiwa kuwa wenyeviti au Marais wa klabu husika.

Nafasi ya Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania inagombewa na klabu za Ligi Kuu pekee.

Uchaguzi huo wa kamati hiyo utafanyika Jumapili Oktoba 15, 2017 jijini Dar es Salaam na unaendeshwa kwa mujibu wa kanuni za Uchaguzi za TFF toleo la 2013.