Wednesday 30 August 2017

Kenya: Jaji wa mahakama ya juu augua kesi ya upinzani kupinga matokeo ya urais ikiendelea

Jaji mmoja wa Mahakama ya Juu nchini Kenya ameugua kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi wa urais ikiendelea kusikizwa.

Kwa mujibu wa Jaji Mkuu David Maraga, ambaye ndiye kiongozi wa mahakama hiyo, Jaji Mohammed Ibrahim, mmoja wa majaji saba ambao wamekuwa wakisikiliza kesi hiyo iliyowasilishwa na kiongozi wa upinzani Raila Odinga alianza kuugua kabla ya vikao vya leo kuanza na alihudumiwa na madaktari.

Kuugua kwake kuliwaacha majaji sita wakisikiliza hoja za pande mbalimbali katika kesi hiyo.

Majaji hao wengine ni Naibu Jaji Mkuu Philomena Mwilu, Prof Jackton Boma Ojwang, Bi Njoki Ndung'u, Isaac Lenaola na Dkt Smokin Wanjala.

Bw Odinga amepinga hatua ya Tume ya Uchaguzi (IEBC) kumtangaza Rais Uhuru Kenyatta kuwa mshindi wa uchaguzi wa urais uliofanyika tarehe 8 Agosti.

Majaji hao wanatarajiwa kutoa uamuzi wao kufikia Ijumaa tarehe 1 Septemba.

Kwa mujibu wa matokeo ya IEBC, Rais Kenyatta alipata kura 8,203,290 huku naye Raila Odinga akipata kura 6,762,224.