Friday 22 September 2017

TCRA yawakumbusha wananchi kutumia vizuri miitandao ya kijamii

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka hiyo, Injinia James Kilaba wakati wa semina ya matumizi bora ya mitandao ya kijamii pamoja na uzinduzi wa kampeni ya kusisitiza matumizi bora ya mtandao awamu ya pili iliyohusisha wamiliki wa blogu Tanzania na waandishi wa habari za mtandaoni iliyoratibiwa na TCRA leo jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa wawasilishaji wa mada katika semina hiyo, makosa mengi ya kimtandao yanayoripotiwa katika vyombo husika yanasababishwa na uchu wa kutafuta pesa hali inayofanya watu kujiingiza katika wizi kwa kutumia mtandao.

Sababu zingine zinazosababisha makosa katika mtandao ni pamoja na kutokuwa na sera madhubuti katika blogu zinazolinda utoaji na upokeaji wa taarifa, baadhi ya wahalifu wanafikiri kuwa kufanya uhalifu katika mitandao ni salama kwao kwa sababu hakuna jicho la serikali, kumbe wanajidanganya.

Sababu nyingine ni kutafuta umaarufu kwa kukimbilia kuonekana wa kwanza kuchapisha habari, kwa uharaka huo kuna uwezekano mkubwa wa kuchapisha makosa mengi kwa kuwa hakuna muda wa kujiridhisha na ukweli na uhakika wa habari husika.

Wananchi wanashauriwa wakipata ujumbe wenye maudhui yasiyofaa waufute haraka na wasiusambaze. Pia kutokana na sheria ya makosa ya mtandao, ikiwa mtu yeyote akitumiwa hela kimakosa asiitoe bali awasiliane na kampuni ya simu husika kwa maelezo zaidi na hatua zaidi.

Vile vile ikiwa mwananchi amepokea ujumbe wa vitisho au matusi kitu cha kwanza ambacho anapaswa kukifanya sio kuujibu ujumbe huo au kuusambaza katika makundi mbalimbali bali ni kuwasilisha ujumbe huo polisi kwa hatua zaidi ili usalama wa aliyepokea ujumbe uwepo.