Wednesday 25 October 2017

Waethiopia 74 wakamatwa Mtwara

Mtwara. Ofisi ya Uhamiaji mkoani Mtwara kwa kushirikiana na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) imewakamata wahamiaji wasiofuata utaratibu 74 raia wa Ethiopia.

Uhamiaji imesema wahamiaji 67 wamekamatwa eneo la Msanga Mkuu wilayani Mtwara wakielekea Msumbiji ikielezwa lengo lao lilikuwa kwenda Afrika Kusini.

Wahamiaji hao waliotokea Mombasa nchini Kenya imeelezwa walikuwa wakiongozwa na raia wa Tanzania kutoka Pemba aliyetajwa kwa jina la Bakari Ally.

Ofisa Uhamiaji Mkoa wa Mtwara, James Mwanjotile amesema kati ya wahamiaji hao 67, ni 14 pekee wenye hati za kusafiria lakini hawakufuata utaratibu wa kupita kwenye ofisi za uhamiaji.

Mwanjotile amesema wahamiaji wengine saba wamekamatwa wilayani Tandahimba.

Amesema wahamiaji wote 74 wamefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Mtwara kwa kosa la kuingia nchini bila ya kufuata utaratibu.