Wednesday 25 October 2017

Kizimbani kwa kutishia kumuua Diwani

WATU nane wakazi wa Ntyuka Manispaa ya Dodoma, wamefikishwa katika Mahakama ya Mwanzo ya Chamwino kwa tuhuma za kutishia kumuua kwa maneno Diwani wa Kata ya Ntyuka, Theobale Emmanuel.

Waliofikishwa kizimbani na kusomewa shtaka hilo ni Edward Lamoli, Edward Lauli, Petro Mjelwa, Yona Andrea, Lucas Mombo, Stephen Karashani, Zabron Leganga na Mussa Majana.

Kesi hiyo namba 234 ya mwaka 2017 inasikilizwa na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo ya Chamwino, Zawadi Ndudumizi.

Ilidaiwa mahakamani hapo kuwa washtakiwa walitenda kosa hilo Ntyuka kinyume cha kifungu cha 89 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu Sura ya 16 ambacho kilifanyiwa marejeo mwaka 2002.

Hata hivyo, Washtakiwa wako nje kwa dhamana na kesi hiyo itasikilizwa tena Oktoba 24 mwaka huu.