Tuesday 24 October 2017

Huyu ndio kiongozi mwenye nguvu zaidi nchini China tangu kipindi cha Mao Zedong'

Chama cha Kikomunisti nchini China kimepiga kura kujumuisha falsafa zake Xi Jinping katika katiba na kumuinua hadi kifikia kiwango alichokuwa nacho mwanzilishi Mao Zedong.

Kura hiyo ya kuunga mkono kuandika fikra zake Xi Jinping, ilifanyika wakati wa kukamilika kwa mkutano mkuu wa chama cha Kikomunisti ambao ndio mkutano mkubwa zaidi wa kisiasa nchini China.

Bw. Xi ameongeza madaraka yake tangu ashike uongozi mwaka 2012.
Hatua hiyo ni ishara kuwa wapinzani wake hawawezi kumpinga bila ya kitishia utawala wa chama cha Kikomunisti.

Mkutano huo wa Komunisti ulianza wiki iliyopita kwa hotuba ya saa tatu ya Bw. Xi. ambapo alielezea falsafa yake ya siasa za ujamaa.

Maafisa wa vyeo vya juu na vyombo vya habari vya serikali walianza kuzungumzia falsafa hiyo wakiitaja kuwa fikra zake Jinping, ishara kuwa Bw. Xi alikuwa ameimarisha ushawishi wake chamani.

Watoto wa shule, wanafunzi wa vyuo vikuu na wafanyakazi katika makampuni ya serikali sasa wataungana na wanachama milioni 90 wa chama cha Kikomunisti, kusoma fikra zake Xi Jinping kuhusu kipindi kipya cha ujamaa.

Ikiwa kwanza alikuwa ni mwenyekiti Mao kuunganisha nchi ambayo ilikuwa imeharibiwa na vita na ya pili, ya China kutajirika nchini ya Deng Xiaoping, kipindi hiki kipya ni cha kujenga umoja zaidi na wakati huo huo kuifanya China kwa na nguvu nje.

Kuyajumuisha haya yote kwa jina la Xi Jinping kwenye katiba ya chama ina maana kuwa washindani hawawezi kupinga Xi, bila ya kutishia chama cha Kikomunisti.

Zaidi ya wajumbe 2,000 walitumia mkutano huo wa wiki nzima kuwachagua wakuu wa chama mikoani, magavana na wakuu wa mashirika yanayomilikiwa na serikali.