Tuesday 24 October 2017

Daktari: Kanumba alikuwa na uvimbe sehemu ya nyuma kwenye ubongo

Dar es Salaam. Daktari bingwa wa uchunguzi wa magonjwa ya binadamu na vifo vyenye kutia shaka, Innocent Mosha kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili ameieleza Mahakama Kuu alichobaini baada ya kuufanyia uchunguzi mwili wa msanii wa fani ya uigizaji wa filamu nchini, Steven Kanumba.

Dk Mosha ambaye ni shahidi wa nne wa upande wa mashtaka katika kesi ya kuua bila ya kukusudia inayomkabili msanii wa fani hiyo, Elizabeth Michael maarufu Lulu amesema walipofungua fuvu walibaini ubongo wa Kanumba ulikuwa umevimba.

Lulu anadaiwa kutenda kosa hilo Aprili 7, 2012, nyumbani kwa marehemu Kanumba, Sinza Vatican jijini Dar es Salaam.

Katika ushahidi wake leo Jumatatu Oktoba 23,2017, Dk Mosha akiongozwa na Wakili wa Serikali, Faraja George mbele ya Jaji wa Mahakama Kuu, Samu Rumanyika ameeleza akiwa kazini alipewa maagizo kuwa anatakiwa kuufanyia uchunguzi mwili uliokuwa umehifadhiwa katika Hospitali ya Muhimbili.

Shahidi huyo amesema katika uchunguzi wa mwili wa Kanumba alibaini kuwepo uvimbe sehemu ya nyuma kwenye ubongo na walipofungua fuvu walibaini ubongo ulikuwa umevimba.

Dk Mosha alipoulizwa na wakili wa mshtakiwa Peter Kibatala juu ya sampuli walizopeleka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali kuhusu hali ya kilevi katika mwili wa Kanumba, amesema hakuwahi kufahamu matokeo ya uchunguzi.

Pia, amesema hafahamu kama Kanumba alijigonga ukutani kwa kuwa hakuwepo eneo la tukio.