Thursday 27 July 2017

TRA yapiga kufuli maduka mkoani Iringa

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imefunga maduka ya wafanyabishara mkoani Iringa wasiotumia mashine za kielektroniki za EFD.


Hatua hiyo imekuja baada ya maofisa wa TRA kufanya ukaguzi wa kushitukiza katika maeneo mbalimbali ya mji wa Iringa na kubaini uwepo wa wafanyabiashara wanaodaiwa kutokuwa na mashine za kutolea risiti za EFD.

Meneja wa TRA Mkoa wa Iringa, Ndg Lampson Tulianje amesema wafanyabishara hao wamekaidi agizo la Serikali la kutakiwa kuwa na mashine kwa zaidi ya miezi mitatu.

“Tumewapa maagizo, tumewahamasisha kwa zaidi ya miezi mitatu lakini bado wamekaidi agizo letu, uamuzi tuliochukua ni kufunga duka na mara atakaponunua tunamfungulia duka lake,”amesema Tulianje .

Tulinje amefafanuaa kuwa lengo la kufikia hatua hiyo ni kuhimiza wafanyabiashara hao kulipa kodi stahiki kwa kutumia mashine hizo ambazo zina uwezo wa kuweka kumbukumbu vizuri za mauzo ya bidhaa zao.

Pia Tulinje ametoa wito kwa wafanyabiashara hao kuacha kushindana na Serikali badala yake kuhakikisha wananunua mashine hizo na kuzitumia kwa kuwa hata gharama wanazotumia zinarudishwa na TRA wakati wa kukadiria kodi zao.

“Rai kwa wafanyabiashara ni vyema wakanunua mashine zitakazosaidia kuweka vizuri kumbukumbiu za mauzo yao na kuisaidia Serikali kukusanya kodi sahihi, zaidi yote mashine hizo zinatolewa bure na TRA kwa kuwa gharama wanazotumia kununulia mashine zitaunganishwa kwenye makadirio ya kodi yao ya mapato,”amesema Tulianje kwenye mahojiano yake na Gazeti la Mwananchi.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabishara mkoani Iringa, Ndg Odilo Ngamiraga amesema wafanyabishara hawajagoma kutumia mashine hizo na kwamba tatizo lipo kwa wasambazaji ambao pindi wanapokwenda huambiwa wasubiri.