Sunday 30 July 2017

SALAMU za Rais wa TFF, Jamal Malinzi Kutoka Gerezani Hizi Hapa

Rais wa TFF anayemaliza muda wake Jamal Malinzi amewatumia salamu viongozi wa TFF na kuwatakia uchaguzi mwema unaotarajiwa kufanyika mwezi Agosti mwaka huu.

Aidha, Malinzi katika salamu hizo, ameishukuru Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dk. John Pombe Joseph Magufuli, wadhamini mbalimbali, washirika na wadau wa soka kwa ushirikiano walioutoa katika kipindi chote cha uongozi wake.

Salamu hizo ambazo zimetolewa kupitiwa kwa mawakili wake zilieleza kuwa anaamini kwamba TFF watafanya uchaguzi vizuri na viongozi watakaopatikana wataweza kuendeleza programu muhimu.
Malinzi alilazimika kujiondoa kwenye uongozi wa TFF na kushindwa kutetea nafasi yake baada ya kuwekwa rumande tangu Juni 29 kwa tuhuma za ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka.

Malinzi, Katibu wake, Selestine Mwesigwa pamoja na Mhasibu wa TFF, Nsiande Isawafo Mwanga walipelekwa rumande Juni 29 baada ya kusomewa mashitaka 28 ya kughushi na kutakatisha fedha kupitia akaunti ya TFF iliyopo katika banki ya Stanbic, Dar es Salaam.