Monday 31 July 2017

Chadema nayo yaanza kutumbua Majipu ya ndani

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), imemfuka aliyekuwa mwenyekiti wa wilaya ya Hai, James Mosha, kufutwa uanachama.

Hali hiyo imetokea siku chache baada ya chama cha Wananchi (CUF) kutangaza kuwafukuza ubunge na uanachama wabunge wanane kwa kile kilichodaiwa kutokuwa na nidhamu dhidi ya mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba, anayetambulika na Msajili wa Vyama vya Siasa.

Aidha, Nkiya amefukuzwa uanachama ikiwa siku chache baada ya madiwani watatu wa chama hicho kujiengua na kujiunga na CCM.

Kaimu Mwenyekiti wa chama hicho, Joel Nkiya, aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa wanalazimika kumfukuza uanachama Mosha kwa madai ya usaliti unaoendelea katika chama hicho na kwamba hawataweza kuuvumilia.

Nkiya alisema Mosha ambaye alikuwa mwenyekiti, alijiuzulu wadhifa wake mwaka jana lakini hakujivua uanachama, hivyo chama kimeafiki kumfukuza kwa kufuata sheria na kanuni za chama hicho kutokana na kueneza nguvu ya usaliti ndani ya chama.

Alisema wanalaani vikali kitendo cha madiwani hao kujiondoa katika chama na kwamba kwanza wameonyesha wasivyo wazalendo na waharibifu wa rasilimali za umma.

"Wanapojiuzulu na kujivua uanachama moja kwa moja wameachia nafasi zao za uongozi. Kutokana na hilo uchaguzi utafanyika tena, hapo ndipo rasilimali za Watanzania zinapotea kwa kukosa uzalendo,” alisema.

Naye Mwenyekiti wa Baraza La Madiwani Hai, Helga Mchomvu, alisema hawana wasiwasi na kuondoka kwa madiwani hao kwa kuwa walikuwa hawana mchango wowote katika utendaji wao wa kazi.

"Madiwani hao waliokuwa wanajiondosha tulikuwa tunatilia shaka utendaji wao na tulianza kuwajadili, hivyo tunawatakia kila la heri huko waliko. Wananchi wanapenda kutazama utendaji na si jina la mtu, hivyo wamejipima wakaona mwaka 2020 wasingerudi kwenye nafasi zao wakaamua kujivua,” alisema.

Mmoja wa madiwani wanaotajwa kutaka kujivua uanachama, Bariki Mbise (Rundugai), alisema kuna mbinu chafu zinazoendelea hasa katika Jimbo la Hai za kuhakikisha mwaka 2020 wananchi wanakosa imani na chama chao,

“Mimi binafsi nimesharubuniwa na kuahidiwa Sh. milion 30. Ningekuwa sina uzalendo na imani kwa wananchi walionichagua tayari ningeshajivua uanachama.

Mmoja wa waliojiuzulu alinifuata na kunishawishi tujiuzulu kwa kiasi fulani cha fedha tumeaidiwa na mtu fulani,” alidai Mbise.