Tuesday 30 May 2017

Spika Ndugai: Natamani kupanda mabasi ya mwendo kasi

Dodoma. Spika wa Bunge, Job Ndugai amesema anatamani kupanda mabasi ya mwendo wa haraka yaliyoko jijini Dar es Salaam.

Pia, ameishauri kampuni ya usafiri ya Udart kuangalia uwezekano wa kuwekeza mjini
Dodoma.

Akizungumza leo (Jumanne) baada ya kukutana na maofisa wa Udart waliomkabidhi majarida ya kutimiza mwaka mmoja tangu kuanza shughuli za usafirishaji, Ndugai amesema siku akifika Dar es Salaam atahakikisha anapanda mabasi hayo, akiwataka wasaidizi wake kumkumbusha ili kujionea jinsi linavyoendeshwa.

Amesema kitendo cha mradi huo mkubwa kuendeshwa na Serikali kwa kushirikiana na mbia ambaye ni Mtanzania ni kielelezo kwamba Watanzania wanaweza.

Ndugai amewataka Udart kuboresha usafiri huo kwa kuongeza mabasi na kampuni hiyo kuangalia namna ya kuwa na mabasi mjini
Dodoma kwa kuwa ndiko yaliko makao makuu ya nchi na watu wameongezeka.

Mkuu wa Kitengo cha Habari Msaidizi wa Udart, Joe Beda amesema watafanya kila linalowezekana kuhakikisha mradi huo unakuwa endelevu kwa kuwa ni
moja ya miradi ya aina yake barani Afrika.