Wednesday 31 May 2017

Huyu Ndiye Bilionea Dangote ..Apanga Kununua Kiwanda Hiki Kikubwa cha Kutengeneza Magari Afrika..!!!

Mfanyabiashara tajiri Afrika, Aliko Dangote anasubiri idhini ya Benki Kuu ya Nigeria ili anunue kiwanda cha kuunda magari aina ya Peugeot akishirikiana na majimbo mawili.

Kampuni ya Usimamizi wa Mali ya Nigeria (AMCON), iliyoundwa wakati wa kuyumba kwa benki, inakaribia kuuza Kiwanda cha Magari cha Peugeot cha Nigeria (PAN).


“Tumeshakamilisha mchakato wote wa zabuni miezi miwili iliyopita na sasa tunasubiri idhini ya Benki Kuu,” alisema ofisa mtendaji mkuu wa AMCON, Ahmed Kuru alipoongea na Reuters.


PAN, kiwanda cha kuunda magari kilichopo jimbo la Kaduna, kina ubia wa kiufundi na PSA Peugeot Citroen na kikiwa na uwezo wa kuunganisha magari 90,000 kwa mwaka.


Dangote, kwa kushirikiana na majimbo ya Kaduna na Kebbi na Benki ya Viwanda (BOI) waliomba zabuni ya kuwa wamiliki wakubwa wa hisa za PAN mwaka jana kutokana na AMCON kutaka kuuza baadhi ya mali zake ilizozichukua wakati wa matatizo ya taasisi za kifedha.