Monday 29 August 2016

VUA NGUO NIKUPE UTAMU!!!!!!!!


Jamani hii sio falsafa ya kaka yangu Simon Mkodo wa Kitururu, kwa hiyo naomba msistushwe na kichwa cha habari hapo juu. Jana nikiwa nimejipumzisha nyumbani baada ya kutoka kanisani, niliamua kufungulia redio ili kusikiliza habari mbali mbali.

Nilipofunga redio nilikutana na kipindi cha watoto kilichokuwa kikirushwa hewani na Redio One, wakati huo ilikuwa ni wakati wa vitendawili, nilijikuta nikivutiwa na kile kipindi kwani kilinikumbusha enzi zile nikiwa mwanafunzi, nilitulia kwenye kiti na kusikiliza kipindi kile.

Mara mwanafunzi mmoja aliyetakiwa kutoa kitendawili chake akasema ‘Kitendawili’
Wenzake wakajibu ‘tega’, na ndipo akasema ‘Vua nguo nikupe utamu’
Yule mwendesha kipindi ambaye alikuwa ni miongoni mwa wale wanafunzi alimkata yule mwanafunzi kalma, na kumuonya yule mwanafunzi, kwa maneno yake mwenyewe alisema, ‘Jamani hivyo vitendawili haviruhusiwi, kwa nini huwaulizi wenzio, muwe mnawaelimisha wenzenu’

Akamchagua mwanfunzi mwingine na kipindi kikawa kinaendelea. Hata hivyo mimi bado nilibaki na swali, Je yule mwanafunzi alimaanisha nini katika kitendawili chake?
Kwa nini hakupewa nafasi ya japo kutoa jibu akiwa Off Air na kisha muongoza kipindi akatoa ufafanuzi? Je watoto walioko majumbani ambao walikuwa wakisikiliza kile kipindi watakuwa na picha gani juu ya kile kitendawili?

Unajua siku hizi kiswahili kimegeuzwa sana kiasi kwamba kila neno siku hizi limegeuka kuwa matusi.

Kwa kawaida watoto ni wadadisi sana na hicho kitendawili huenda watoto wengine waliokuwa kwenye kipindi na wale waliokuwa wakisikiliza majumbani mwao wamewauliza wazazi wao, na kwa bahati mbaya sana mwenye jibu la kitendawili kile alinyimwa haki ya kutoa jibu, Je wazazi watajibu nini?

Mpaka leo bado natafuta jibu la kitendawili kile, mwenye nalo anisaidie……