Wednesday 6 April 2016

Waheshimiwa Wamrejesha Profesa Jay kwenye Gemu

Mbunge wa Jimbo la Mikumi, Morogoro na rapa nguli nchini, Joseph Haule ‘Prof Jay’ amesema licha ya kuwa na wadhifa wa ubunge, bado ataendeleza fani yake ya muziki kwa kile alichosema hata waheshimiwa wenzake wamemtaka kuendelea hivyo.
Mkali huyo asiyechuja kwenye gemu ya muziki akifafanua kauli yake amesema amekuwa akipigiwa kelele na mashabiki wake wakiwemo wabunge na viongozi wa juu kabisa kutoacha muziki, hivyo lazima asikilize vilio vyao.
Anaongeza kuwa hata isingekuwa vilio vyao, bado mpango wa kukacha gemu haukuwepo kwani ndiyo asili yake na uliompa kila kitu anachojivunia kwa sasa.
“Muziki ndiyo umelea familia yangu, umaarufu wangu na hiki cheo pia ni kutokana na kile ninachokiimba kwenye muziki. Nilichokuwa nakiimba sasa nataka kukifanya kwa vitendo.
“Kiukweli siyo kusema utakuwa ni muziki wa kiushindani, kwamba nionekane kwenye shoo kama mwanzo ama ‘back to back’ ila watapata burudani kwa mfano kupitia ‘interview’ na aina nyingine. Hii ni kutokana na kubanwa na majukumu ya kuwatumikia watu wa jimbo langu,” alisema Jay ambaye alitamba na vibao vingi kama Niamini, Hapo Vipi.